Habari

WIZARA YA ARDHI YASHIKA NAFASI YA KWANZA KUNDI LA WIZARA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI   

  • 03 Oct, 2023
WIZARA YA ARDHI YASHIKA NAFASI YA KWANZA KUNDI LA WIZARA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI   

Na Munir Shemweta, WANMM

Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imekabidhiwa tuzo ya ushindi wa kwanza kwa upande wa kundi la Wizara iliyofanya vizuri katika kutekeleza uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Tuzo hiyo iliyotolewa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) imekabidhiwa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kwa Waziri wa Ardhi Mhe. Jerry Silaa tarehe 2 Oktoba 2023 wakati wa ufungaji Kongamano la Saba la Uwezeshaji Kiuchumi katika ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

Akizungumza kwenye kongamano hilo, Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa amewataka Viongozi na Watendaji Wakuu wa Taasisi za Umma na Sekta Binafsi kuimarisha huduma za uwezeshaji ili kufikia malengo waliojiwekea na kutimiza dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza uwezeshaji na kupunguza umaskini nchini.

ametoa miezi mitatu kwa Wakuu wa Mikoa yote nchini ambao bado hawajaanzisha vituo vya uwezeshaji wananchi kiuchumi kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020/2025 wawe wameshaanzisha kabla ya mwaka 2024.

Awali, Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Beng'i Issa alisema kongamano hilo linalenga kuongeza ufahamu wa wadau mbalimbali kuhusu dhana ya uwezeshaji wananchi kiuchumi na kuwakumbusha majukumu waliyonayo katika kuwawezesha Watanzania.

Alisema malengo mengine ni pamoja na wadau kupeana uzoefu katika kutekeleza shughuli za uwezeshaji wananchi kiuchumi, kuzindua taarifa ya mwaka 2022/2023 ya utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004 ambayo pia imejumuisha masuala ya ushiriki wa Watanzania katika miradi ya kimkakati na uwekezaji unaofanyika nchini.