Habari

WAZIRI SILAA AMKABIDHI DIAMOND HATI TATU ZA ARDHI

  • 27 Feb, 2024
WAZIRI SILAA AMKABIDHI DIAMOND HATI TATU ZA ARDHI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Jerry Silaa amemkabidhi Msanii wa kizazi kipya Nasibu Abdul (Diamond Platnum) hati za umiliki wa viwanja vitatu anavyovimiliki katika maeneo mbalimbali jijini Dar es salaam.

 

Makabidhiano hayo yamefanyika katika viwanja vya shule ya Msingi Bunju "A" Februari 22, 2024 jijini Dar es salaam ambapo Kliniki ya Ardhi inaendelea.

 

Akizungumza mara baada ya kukabidhi hati hizo Waziri Silaa amewahamasisha wananchi maeneo mbalimbali nchini kujitokeza kumiliki viwanja vyao kwa kufuata utaratibu wa umilikishaji hadi kukabidhiwa hati zao.

 

Kwa upande wake Msanii Diamond ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na ubunifu wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuja na wazo la Kliniki ya Ardhi ambayo inawasaidia watu kupata hati zao kwa muda mfupi tofauti na mchakato wa awali ambao ulikuwa unatumia muda mrefu zaidi kupata hati. 

 

Aidha, Msanii Diamond amewasihi wasanii nchini, watumie fursa hii inayotolewa na Wizara ya Ardhi kwa kuendesha Kliniki ya Ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ili wapate hati za viwanja vyao na kukuza uchumi wao.

 

Zoezi la Kliniki ya Ardhi kwa wakazi wa Wilaya ya Kinondoni linaloendelea katika viwanja vya Shule ya Msingi Bunju "A" jijini Dar es salaam limeanza Februari 19 na litahitimishwa Februari 28, 2024 na baadae kuahamia Kata ya Mwenge katika mkoa wa Dar es salaam Dar es salaam.