Habari

WAKUMBUSHENI WAUMINI KUSIMAMIA HAKI NA KUDUMISHA AMANI-DKT MABULA

  • 28 Jun, 2023
WAKUMBUSHENI WAUMINI KUSIMAMIA HAKI NA KUDUMISHA AMANI-DKT MABULA

WAKUMBUSHENI WAUMINI KUSIMAMIA HAKI NA KUDUMISHA AMANI – DKT MABULA

Na Munir Shemweta, WANMM

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angeline Mabula amewataka viongozi wa dini nchini kuwakumbusha mara kwa mara waumini pamoja na watu wote umuhimu wa kusimamia haki na kudumisha amani.

Dkt Mabula alisema hayo wakati akifungua Siku Kuu za Makambi za Kanisa la Waadventista Wasabato Mtaa wa Magomeni Mwaka 2023 iliyofanyika Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam.

‘Amani ni suala muhimu na bila amani hakuna maendeleo hivyo basi hatuna budi kusimamia haki, kuenzi pamoja na kuitunza amani yetu kwa manufaa yetu na vizazi vijavyo’’ alisema Dkt Mabula.

Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi aliyekuwa Mgeni rasmi kwenye Ufunguzi huo wa Makambi mwaka 2023, kwa sasa dunia imekuwa na mabadiliko makubwa mengine yakiendana na mafundisho ya dini huku mengine yakiwa  hayamtukuzi mungu  na kutolea mfano jinsi ya mioyo ya watu ilivyobadilika.

‘’Wivu, chuki, husuda na mambo ya aina hiyo yanachangia kusambaratika kwa familia, marafiki na hata jamii kwa ujumla na mambo hayo yameongezeka sana, wakati mwingine mambo kama haya yanafikia kuleta mauaji katika jamii’’ alisema Dkt Mabula.

Alitoa rai kwa madhehebu ya dini kuelekeza kufundisha yaliyo mema ili jamii ifuate mapenzi ya mungu na kuepuka kujiingiza kwenye machukizo kwa mungu huku akilishukuru Kanisa la Waadventista Sabato Tanzania kwa kuweka wazi msimamo na masharti kwa yale mambo yanayoenda kinyume na maadili ya mtanzania na kubainisha kuwa msimamo huo ukifuatwa  utalisaidia kanisa  na jamii kwa ujumla.

Aliwaomba viongozi hao wa dini kutochoka kufundisha na kulea vijana katika maadili mema pamoja na kuthamini kufanya kazi halali huku akitahadharisha kuwa kushuka kwa maadili ni jambo lenye athari mbaya kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Waziri wa Ardhi, aliwataka viongozi wa dini kusaidia kulea vijana kwa sababu wao wao ndiyo wahanga wakuu wa maovu  yanayotendeka lakini pia wao ndiyo taifa la leo na viongozi na wachungaji wa kesho.

‘’Tukiwandaa vyema vijana, mustakabali wa Taifa letu na watu wake utakuwa kwenye mikobno salama tu, tukishindwa leo tutalia na kusaga meno’’ alisema Dkt Mabula.

Kanisa la Waadventista Sabato Magomeni limekuwa na utaratibu wa kuwa na Makambi kila mwaka kwa lengo la kutoa mafundisho kwa waumini wake na kwa mwaka huu wa 2023 mkutano huo umebeba ujumbe usemao ‘NITAKWENDA KUJIHUSISHA

Katika hatua nyingine, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ameshiriki kupanda miti eneo la uwekezaji la Kanisa Waadentista Sabato lenye ukubwa wa ekari 20 lilipo Kwembe Dar es Salaam. Kwa mujibu wa Israel Kamuzora ambaye ni mmoja wa Wazee wa Kanisa hilo, uwekezaji utakaofanywa eneo hilo utahusisha mambo mbalimbali kama vile kuwa na Ukumbi, Hosteli, Shule za Muziki, Makumbusho ya Kanisa, Chuo cha Mapishi Bora, Hospitali ya Mama na Mtoto pamoja na Maktaba kubwa ya Kanisa.

‘’Eneo hili tutalitumia kama eneo la uwekezaji wa Kanisa letu maana tutajenga ukumbi wa mkutano wenye uwezo wa kuchukua watu 3,000, Hostel watu 500, Shule ya Muziki pamoja na eneo la Makumbusho’’ alisema Kamuzora.

Kwa upande wake Waziri wa Ardhi Dkt Mabula amelipongeza Kanisha la Waadventina Sabato kwa kwa jitihada mbalimbali inazofanya ikiwemo kuwa na malengo ya kuanzisha uwekezaji eneo la Kwembe alioueleza kuwa, utakaposimamiwa vizuri kwa kiasi kikubwa utagusa wananchi.