Habari

SILAA ATAKA MAENEO YA HUDUMA KUPIMWA NA KUPATIWA HATI

  • 10 Oct, 2023
SILAA ATAKA MAENEO YA HUDUMA KUPIMWA NA KUPATIWA HATI

Na Munir Shemweta, WANMM TABORA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jerry Silaa amewataka wakurugenzi wa halmasahauri nchini kuhakikisha maeneo yote ya huduma za jamii yanapimwa kwa lengo la kulinda maeneo hayo.

Waziri Silaa amesema hayo tarehe 9 Oktoba 2023 mkoani wakati akizungumza na uongozi pamoja na watumishi wa sekta ya ardhi mkoa wa Tabora akiwa kwenye ziara yake ya kufuatilia utekelezaji wa Maamuzi ya Baraza la Mawaziri Kuhusiana na utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975.

'' Ni vyema wakurugenzi wote wa halmashauri wakapima maeneo yao ya huduma za jamii ili waweze kuyalinda kwa vizazi vya sasa na vile vinavyokuja'' alisema

Amesema, kwa sasa ndani ya wizara yake kuna mabadiliko wanayokwenda kuyafanya katika maeneo yanayoonekana kama kikwazi kwa sekta hiyo na kutolea mfano wamiliki wa ardhi kuogopa kuchukua hati kwa hofi ya kulipa kodi ya ardhi sambamba na uwezo wa kifedha baadhi ya halmashauri katika kutekeleza majukumu ya sekta ya ardhi.

''Kwa hiyo tunaenda kufanya mabadiliko mazuri tunayoamini yakifanyika yatasaidia sekta ya ardhi kuendelea kusaidia sekta nyingine kwa kuwa sekta ya ardhi ni sekta mtambuka''. alisema

Aidha, ameweka wazi kuhusu suala la usimamizi wa sheria za ardhi ambapo amesema halmashauri zimekuwa na msukumo mkubwa kutoka kwa wananchi kuhusu suala hilo ambapo amesema hakuna msukumo unaopelekea uvunjifu wa amani na kusisitiza kuwa maeneo ya wazi yabaki wazi na yale ya huduma kama taasisi yabaki kuwa ya taasisi.

''tumekubalina maeneo yote ya huduma, mashule, vituo vya afya, zahanati yapimwe na yapate hati na mfikishe salama zangu kwa wakurugenzi maeneo yote ya huduma yapimwe na yapate hati.

Aidha, katika ziara hiyo waziri Silaa amehimiza pia suala la usimamizi wa sheria katika kutekeleza majukumu sambamba na kuziagiza mamlaka za uhifadhi nchini kuhakikisha zinaongeza nguvu katika kulinda maeneo ya hifadhi ili wananchi wasiweze kuvamia maeneo hayo.

''Mimi naamini kabisa maeneo mengi viongozi wanapenda kuhakikisha haki za wananchi zinapatikana na tunapoendekeza wanaovunja sheria tunawavunja nguvu wale wananchi kwa kufuata na kuzingatia sheria'' alisema Silaa.

Waziri Silaa amehitimisha ziara yake ya siku moja katika mkoa wa Tabora ambapo mbali na kuzungumza na watumishi alipata fursa ya kutembelea ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Tabora, Chuo cha Ardhi Tabora pamoja na kitega uchumi cha Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).