Habari

SERIKALI YAWAHIMIZA WANAWAKE KUMILIKI ARDHI

  • 21 Jun, 2026
SERIKALI YAWAHIMIZA WANAWAKE KUMILIKI ARDHI

Serikali imewahimiza wanawake kujitokeza kumiliki ardhi na kutumia fursa zilizowekwa kwa kupitia Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995, Toleo la mwaka 2023 ili kuendelea kunufaika na fursa zinazopatikana kupitia sekta ya Ardhi nchini.

 

Sera hiyo ambayo ilizinduliwa mwezi Machi 17, 2025 na Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasisitiza usawa wa kijinsia katika upatikanaji, umiliki na matumizi ya ardhi na imeondoa vikwazo vya mila na tamaduni ambazzinaathiri upatikanaji sawa wa haki ya kumiliki ardhi kwa Wanawake

 

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Lucy Kabyemera ameyasema hayo wakati alipotembelea banda la Wizara hiyo katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

 

Amesema kuwa Serikali kupitia sera, sheria na mifumo mbalimbali ya usimamizi wa ardhi imeendelea kuimarisha ushiriki wa wanawake katika umiliki wa ardhi na kuondoa vikwazo vinavyoweza kuwanyima haki hiyo.

 

“Umiliki wa ardhi unawawezesha wanawake kiuchumi, unaimarisha usalama wa makazi na kuongeza uwezo wao wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na maendeleo ya familia na Taifa kwa ujumla” amesisitiza Naibu Katibu Mkuu Bi. Kabyemera.

 

Kupitia maonesho hayo, Wizara hiyo inatoa huduma mbalimbali kwa wananchi ikiwemo ushauri wa kisheria kuhusu masuala ya ardhi, kuhuisha hatimiliki zilizoisha muda wake pamoja na utoaji wa hati miliki papo kwa papo kwa wananchi waliokamilisha taratibu zote za umilikishwaji wa ardhi.

 

Katika hatua nyingine, Bi. Kabyemera amewataka wananchi wote nchini kuhakikisha wanalipa kodi ya pango la ardhi kwa wakati kuepuka kutozwa riba na adhabu kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili kuongeza mapato ya Serikali kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.

 

Nae Bi. Julieth Msuya ameipongeza Serikali kwa kuendelea kusogeza huduma kwa wananchi kwa kupitia maonesho hayo ambapo amefanikiwa kupata hati yake.

 

“Kupitia maonesho haya nimefanikiwa kupata hati yangu ambayo itanisaidia kuongeza ulinzi katika eneo langu’’ amesema Bi Msuya.

 

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2026 yanaongozwa na kaulimbiu "Kukuza Matumizi ya Mifumo ya Kidijitali ili Kuongeza Upatikanaji wa Taarifa na Kuchagiza Uwajibikaji" ambapo yalianza Juni 16, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026 katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.