Habari

MIGOGORO YA ARDHI DODOMA YAMPELEKA NAIBU WAZIRI PINDA UWANDANI

  • 15 Jan, 2024
MIGOGORO YA ARDHI DODOMA YAMPELEKA NAIBU WAZIRI PINDA UWANDANI

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geophrey Pinda ameingia uwandani kutatua na kufuatilia utekelezaji wa maagizo yake ya migogoro ya ardhi katika jiji la Dodoma.

 

Mhe Pinda katika ziara yake hiyo tarehe 11 Januari 2024 aliambatana na watendaji wa sekta ya ardhi Makao Makuu ya Wizara, Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma na wale wa Jiji la Dodoma ambapo alitembelea eneo la Chang'ombe.

 

Naibu Waziri wa Ardhi alianza ziara yake kwa kutembelea eneo la Chang'ombe Mbwanga ambapo Bi Dorothy alibomolewa kimakosa ukuta wa nyumba yake na halmashauri ya jiji la Dodoma ambapo Mhe. Pinda alielekeza mwananchi huyo kujengewa ukuta huo.

 

''Ninyi mnaoishi hapa sura ya ujirani lazima itengenezwe kwa kuepuka migogoro ya ardhi katika maeneo yenu, mnataka mpaka waziri aje ndiyo atengeneze ujirani'' alisema Mhe. Pinda

 

Aidha, alitembelea eneo la Chang'ombe Extension, ambapo mwananchi mmoja Ramadhani Kisiju anadai kumiliki kiwanja alichokuwa akilima kwa muda mrefu.

 

Katika kutafuta suluhu ya eneo hilo, Mhe Pinda aliagiza mmiliki wa eneo analodai Kisiju kumiliki afiki ofisini kwake na nyaraka zote za umiliki kwa lengo la kupata muafaka wa mgogoro huo.

 

''Kitu kimoja ninachotaka kukusaidia mzee wangu, ngoja tukaangalie hiki kiwanja uhalali wake halafu baadaye tutakupa majibu'' alisema Naibu Waziri wa Ardhi.

 

Uamuzi wa Mhe Pinda kutembelea na kukagua maeneo ya mgogoro uwandani unafuatia kuwasilishwa kwa malalamiko ya migogoro ya ardhi kwake huku baadhi ya malalamiko yakihusisha watendaji wa sekta ya ardhi.