Habari

MAJALIWA ATAKA WAVAMIZI WA ARDHI KUCHUKULIWA HATUA KAMA JINAI NYINGINE

  • 24 May, 2024
MAJALIWA ATAKA WAVAMIZI WA ARDHI KUCHUKULIWA HATUA KAMA JINAI NYINGINE

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kasim Majaliwa Majaliwa amezitaka taasisi zinazoshughulika na masuala ya ya jinai kuhakikisha zinachukua hatua dhidi ya wavamizi wa ardhi kama jinai nyingine.

 

Mhe. Majaliwa ametoa kauli hiyo leo tarehe 23 Mei 2024 katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba na  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Klinik ya Ardhi katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

 

"Taasisi zote zinazoshughulikia jinai ziendelee kuchukua hatua dhidi ya uvamizi wa ardhi kama jinai nyingine na suala hilo lishughilikiwe kwa haraka" amesema Mhe Waziri Mkuu.

 

Kwa mujibu wa hotuba hiyo ya Waziri Mkuu,  Maelekezo hayo yanatokana na ukweli kuwa,  wapo baadhi ya wananchi wanakiuka sheria kwa makusudi kwa kuvamia maeneo yenye miliki halali tena wakati mwingine yana miliki za watu wanyonge na kutumia madaraka na nguvu na madaraka kupora milki za ardhi za watu wengine.

 

"Wakati mwingine maeneo yenye umiliki halali ya taasisi za umma pia yamekuwa yakiporwa na kutumika kinyume cha sheria na taratibu za nchi". Amesema.

 

Amebainisha kuwa, Kuachiwa kwa jinai kuendelea ni kukuza migogoro ambayo inajihusisha na uvamizi wa ardhi katika maeneo mbalimbali nchini. 

 

Hata hivyo, amezitaka taasisi zote zinazomiliki ardhi kuendelea kuwasiliana na wizara ya ardhi Nyumba na maendeleo ya makazi kwa lengo la kupata uhakika wa umilki na kama upo uvamizk basi hatua zichukuliwe kwa haraka huku akiwataka  wabunge kuisaidia wizara hisusan katika ukiukwaji wa taratibu.

 

Akigeukia Klinik ya Ardhi aliyoizindua, Mhe Mjaliwa amesema, Kutokana na  uendeshaji  wa zoezi la kliniki ya ardhi kuwa na ufanisi mkubwa katika utoaji huduma kwa uwazi na kwa haraka, Wizara iendele kutekeleza  kliniki katika Mikoa na Wilaya zingine nchini.

 

Aidha, ameitaka wizara kuboresha mifumo itakayowawezesha wananchi kutumia mifumo kuomba na kufuatilia huduma zao za ardhi wanazozihitaji, kuongeza uwazi na kasi ya utatuzi wa migogoro pamoja na Kuondoa urasimu na ucheleweshaji usio wa lazima wa utoaji wa huduma inayoombwa kutoka kwa wananchi.

 

Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Jerry Silaa amesema, uzinduzi  wa maonyesho ya Klinik ya Ardhi ni mpango mkakati wa Wizara katika kuhakikisha kuwa wananchi wote wenye uhitaji wa huduma au wenye changamoto za ardhi wanapatiwa huduma na kushughulikiwa katika maeneo yeo na kwa haraka zaidi. 

 

Mhe, Silaa amesema zoezi la Klinik ya Ardhi huendeshwa kwa kuwa na vituo jumuishi vya pamoja sehemu moja za wataalam wote wa sekta,ambao huhama kwa muda kwenye vituo vyao vya kawaida vya ofisi na kwenda kwenye kata au mitaa na kisha kutoa huduma husika za ardhi kama vile uandaaji na usajili wa hatimilki, huduma za upekuzi wa hati, uhamisho wa milki,ukadiriaji na ulipaji kodi ya pango la ardhi, elimu ya masuala ya ardhi na utatuzi wa migogoro  ya ardhi pale kwenye kituo ambacho kliniki ilipo.