Habari
DKT. AKWILAPO NA NAIBU WAKE WAWASILI WIZARANI MARA BAADA YA KUAPISHWA
- 18 Nov, 2025
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo pamoja na Naibu wake Mhe. Kasper Mmuya, leo Novemba 18, 2025 wamewasili rasmi ofisi za Wizara ikiwa ni mara tu baada ya kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kushika wadhifa huo.
Viongozi hao wawili walipokelewa kwa furaha na menejimenti, viongozi wa taasisi zilizo chini ya wizara pamoja na watumishi wa makao makuu ambapo Waziri Mhe.Dkt Leonard Akwilapo amemshukuru Rais kwa kumuamini na kumpa dhamana ya kuiongoza wizara hiyo.
Amepongeza pia tukio la kikao cha kwanza cha utambulisho, akisisitiza kuwa sasa ni wakati wa kushirikiana kwa karibu na kutekeleza majukumu kwa ufanisi mkubwa.
“Mhe. Rais amesisitiza kazi, utu na maendeleo. Tufanye kazi kwa moyo, kwa kufuata taratibu za huduma bora kwa wateja, kwa ubora uleule na ndani ya muda unaotakiwa,” amesema Dkt. Akwilapo.
Aidha, amekumbusha umuhimu wa kufanya kazi kwa kuzingatia staha, kujali muda na kutoa huduma zenye tija kwa taifa.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi, Bw. Kaspar Mmuya, amesema yupo tayari kushirikiana kikamilifu na uongozi wa wizara katika kujenga dira ya pamoja. Amewaomba watumishi kumuunga mkono ili kwa pamoja wafanikishe malengo ya wizara na ya serikali kwa ujumla.