Habari

NAIBU WAZIRI PINDA AMALIZA MGOGORO WA ARDHI KIEGEYA MOROGORO

  • 06 Dec, 2023
NAIBU WAZIRI PINDA AMALIZA MGOGORO WA ARDHI KIEGEYA MOROGORO

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Geofrey Pinda amemaliza na kuufunga wa wananchi 767 wa Kiegeya mkoani Morogoro.

 

Wananchi hao ni wale waliovamia na kulima katika shamba la Tungi Sisal Estate la Mwekezaji Star Infrastructure.

 

Mhe Pinda amemaliza na kuufunga mgogoro huo tarehe 5 Desemba 2023 alipokutana na wawakilishi wa wakulima wakioongozwa na Mwenyekiti wao Haleluya Minga katika ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Morogoro.

 

Naibu Waziri wa Ardhi alifika mkoani Morogoro kwa ajili ya kuwasikiliza ili kupata ukweli ambapo baada ya kuwasikiliza kwa takriban saa nne alibaini udanganyifu katika maelezo ya wakulima na kuwapa taarifa kuwa mwekezaji ni mmiliki halali na alitoa ekari 4000 alizoombwa na serikali na wao wamevamia sehemu mpya.

 

''Niwatake muwe waungwana na mfuate taratibu za kisheria za kupata ardhi na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wale wakataokaidi maelekezo ya serikali na mgogogoro huu kuhusu wananchi 767 nimeufunga rasmi'' alisema Pinda

 

 ''Kesi yenu ilipitiwa katika ngazi mbalimbali na utafiti wake umefanyika mpaka uwandani na kuonesha kuwa ninyi hamna haki, kwanza mko tofauti na idadi yenu inaongezeka kila siku kutoka 319 hadi 767 na bado inaendelea hivyo katika mazingira ya kawaida inawawia vigumu kuwasaidia'' alisema Mhe. Pinda.

 

Mwenyekiti wa wakulima hao Haleluya Minga mbali na kumshukuru Naibu Waziri kwa kuamuzi wake wa kwenda kuwasikiliza wakulima hao alimueleza kuwa, kuongezeka kwa idadi ya wakulima kulitokana na wao kutokuwa na utaratibu wa vikao na baada ya kugundua hilo ndipo walipokutana na kuchagua uongozi.

 

''Kupanda kwa idadi ya wakulima kutoka 319 hadi 767, kwanza hatukuwa na utaratibu wa viakao na tulikuwa hatufahamiani na ilifika mahali kulikuwa na ongezeko tukaamua kuwa na uongozi wa pamoja'' alisema Haleluya.

 

Hata hivyo, Naibu Waziri Pinda amewataka wakulima hao kuwa watulivu na matumizi ya nguvu hayatasaidai kwa kuwa kamati ya mkoa, ofisi ya mkurugenzi wa manispoaa ya Morogoro na ile ya Taifa zinethibitisha kuwa wao siyo wamiliki halali wa maeneo hayo.

 

Awali Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Morogoro Frank Minzikunte alieleza historia ya shamba hilo kuwa inaanzia mwaka 1951 kwa kumilikishwa kwa Mwekezaji na mwaka 1983 serikali ilimuomba mwekezaji ekari 4000 kwa muda ili wananchi wafanye kilimo cha kufa na kupona.

 

Aliongeza kuwa, mwaka 2021 serikali ilimuomba mwekezaji kuziachia moja kwa moja ekari hizo ambapo baada ya majadiliano ya muda mrefu mwekezaji aliridhia na wananchi waliokuwa wamepewa mwaka 1983 wakatambuliwa na takriban wananchi 3777 walitambuliwa na kuingia mkataba na halmashauri ya upimaji shirikishi kama ilivyoelekezwa na serikali.

 

Hata hivyo, Kamishna huyo wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Morogoro alisema, wakati kutambua wananchi hao lilijotokeza kundi la wananchi 319 waliodaia kulima nje ya ekari zilizotolewa na mwekezaji kwa wakulima na ndipo serikali kupitia Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi iliunda tume kwa ajili ya kusikiliza malalamiko pamoja na kero nyingine zinazowakabili wananchi katika ekari 4000.