Habari

HATI 8,325 ZATOLEWA KWA WANANCHI KUPITIA KLINIK YA ARDHI DAR ES SALAAM

  • 18 Mar, 2024
HATI 8,325 ZATOLEWA KWA WANANCHI KUPITIA KLINIK YA ARDHI DAR ES SALAAM

Jumla ya hati 8,325 zimesajliwa na kutolewa kwa wananchi waliofika kupata huduma katika Klinik za Ardhi mkoa wa Dar es Salaam.

 

Aidha, wananchi 18,224 wamefika katika klinik ya ardhi kupata huduma mbalimbali mkoani humo.

 

Hayo yamebainishwa tarehe 17 Machi 2024 na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, Jerry Silaa wakati wa ziara ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii kukagua utekelezaji mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za ardhi (LTIP) katika mkoa wa Dar es Salaam.

 

Amsema, katika Klinik Hiyo migogoro mbalimbali imetatuliwa ikiwemo migogoro ya  mipaka, mirathi, matumizi ya ardhi pamoja na migogoro ya umiliki wa ardhi.

 

Kwa mujibu wa Silaa, Serikali kupitia wizara ya ardhi imeendelea kuchukua hatua za makusdi ili kuhakikisha kuwa utoaji wa huduma za ardhi unaboreshwa kupitia mradi wa uboreshaji Usalama wa Milki za ardhi.

 

Amezitaja hatua zinazochukuliwa kuwa ni kuunda timu za wataalamu wa ardhi katika ngazi za mitaa kwa ajili ya kukwamua kazi za urasimishaji wa makazi katika maeneo yaliyopangwa pamoja na kuendesha Klinik za ardhi katika maeneo mbalimbali.

 

Hatua nyingine ni kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya ardhi kupitia vipindi vya redio na telebisheni, mikutano ya wananchi katika mitaa yao sambamba na kuunda timu za kushughulikia kero na migogoro ya ardhi.

 

Mhe. Silaa ameweka wazi kuwa, azma ya wizara yake ni kuendelea kufanya mageuzi kwenye sekta ya ardhi yanayolenga kuboresha huduma za ardhi kwa maslahi ya wananchi na taifa kwa ujumla.

 

Akielezea zaidi kuhusu Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP), Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amesema, mradi huo ni miongoni wa nyenzo muhimu zilizoonesha mafanikio makubwa katika kuongeza usawa wa kijinsia katika umiliki wa ardhi.

 

''Kati ya Hatimiliki 8325 zilizosajiliwa katika mkoa wa Dar es Salaam Hatimiliki 2,461 sawa na asilimia 29.6 ni za wanawake'' alisema Mhe, Silaa

 

Amefafanua kuwa, mradi huo wa uboreshaji milki za ardhi umewezesha kuongezeka kwa idadi ya wanawake wanaomiliki ardhi nchini kutoka asilimia 25 hadi asilimia 41 huku idadi ya hati za pamoja baina ya wana ndoa zikiongezeka na kufikia asilimia 10 ya hati zilizotolewa.

 

Aidha, amesema Klinik za Ardhi zinazoendeshwa kupitia mradi wa LTIP zimekuwa jukwaa muhimu la kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa wanawake kumililki ardhi.

 

Kwa upande wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kupitia Mwenyekiti wake Mhe. Timotheo Mzava mbali na kuridhishwa na utekelezaji mradi wa LTIP imeipongeza Wizara ya Ardhi kwa kazi nzuri ya kutekeleza miradi ya uboreshaji miliki za ardhi hususan katika klinik za ardhi.

 

''Mnafanya kazi nzuri na sisi kama kamati tunaridhika na kazi inayofanyika na ki ukweli ni kazi ni nzuri na tunataka iendeleee'' alisema Mhe. Mzava

 

Aidha, Kamati imemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anaayoifanya ikiwemo kuwezesha upatikanaji fedha za mradi wa LTIP ili kusaidia utatuzi wa changamoto katika sekta ya ardhi.

 

Aidha, amemtaka Waziri wa Ardhi kuijenga taasisi ili muelekeo alio nao uende mpaka kwa watumishi wa chini kwa kuwa haitatosha maono aliyo nayo kubaki kwa viongozi pekee. ''Huwezi kuwa kila mahali lazima kuwemo mfumo wa kitaasisi utakaoshuka mpaka kwa watendaji wa chini na wimbo uende mpaka ngazi za chini na likifanikiwa hilo tutakwenda vizuri sana''. Alisema Mhe, Mzava

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii mbali na kukagua utekelezaji mradi wa uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) ilishiriki pia kwenye utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa wananchi wa eneo la Bunju Dar es Salaam.